Msemaji wa Wizara ya Ulinzi ya Iran amesema: Leo hii, vikosi vya Jeshi la Iran vinamiliki vifaa vya teknolojia ya juu zaidi ya ulinzi na ndege zisizo na rubani (droni).
Shirika la habari la Mehr limemnukuu afisa huyo wa Jeshi la Iran akieleza kuwa, "Sekta yetu ya ulinzi imefikia hatua ambapo zaidi ya aina 900 za mifumo ya ulinzi na silaha za kisasa imezalishwa nchini."
Kabla ya Mapinduzi ya Kiislamu, Iran ilikuwa na zana 31 pekee za kiulinzi, ameendelea kusema na kuongeza kwamba, mafanikio hayo yanatoka na jitihada za vijana na wanafunzi wa Vyuo Vikuu vya Kiirani.
Ameeleza bayana kuwa, Jamhuri ya Kiislamu imefikia kiwango hiki cha uwezo wa kiulinzi, na daraja yake ya kisayansi imepanda kwa nafasi 40 duniani kote, na sasa ipo katika nafasi ya 16.
Hivi karibuni, Jeshi la Iran lilizindua mfumo mpya wa kukabiliana na makombora ya balestiki wa 'Arman' na vile vile mfumo wa ulinzi wa anga wa “Azarakhsh”.
Uzinduzi wa mifumo na vifaa hivyo vya ulinzi ni matokeo ya juhudi za wanasayansi na wataalamu wa viwanda vya ulinzi vya majeshi ya Iran pamoja na kampuni za sekta binafsi, na vituo maalum vya Vikosi vya Ulinzi vya Iran.
Ifahamike kuwa, doktrini ya kiulinzi ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran imejengeka katika msingi wa kutegemea uwezo mkubwa wa nguvu kazi ya ndani ya nchi.
342/
Your Comment